Sunday, 27 May 2012

Lau ingeuzwa hewa

Kahari Mola Manani, Muumba wetu wadudi
Kwako twapomoka chini, kusudi tukuabudi
Umeijaza angani, hewa isioidadi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

Matajiri duniani, bahili walivyozidi
Wangeitia chupani, hewa kisha wainadi
Hewa I moto thumni, na pauni ya baridi
Mafakiri wangewaje. Lau ingeuzwa hewa

Wangelia masikini, kulilia yao sudi
Hasa kwa bei sokoni, ipandishwapo zaidi
Kungezagaa huzuni, na mauko ya fuadi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

Na makwasi madukani, wangeiuza na kodi
Uwapo huna hunani, kununua huna budi
Mana watoto nyumbani, wanakungoja urudi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

Ingetiwa na melini, iuzwe nchi baidi
Ijengewe juu chini, mabohari ya hadidi
Bora yao ni mapeni, iende yao miradi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

Masikini uwanjani, wangepigishwa paredi
Wapige magoti chini, kusujudia malodi
Ndipo itiwe chupani, warushiwe ja samadi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

Elakini Rahamani, achukiaye husudi
Pembe zote duniani, hewa amejaza hadi
Bure waja pumueni, bila malipo kufidi
Mafakiri wangewaje, lau ingeuzwa hewa

No comments:

Post a Comment